
Meneja wa UpEnergy Tanzania, Jacqueline Ngulla (kulia), akifuatiwa na William Davidson, Mkurugenzi wa Freepoint, pamoja na Giu Warren na James Burrows, walipotembelea Ofisi ya Makamu wa Rais, Mtumba – Dodoma, kwa ajili ya kujadiliana kuhusu fursa za biashara ya kaboni na kuimarisha juhudi za utunzaji wa mazingira na maendeleo endelevu.

Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda (kushoto) akizungumza na wadau wa Mazingira leo tarehe 15 Aprili 2026 katika Ofisi za Makamu wa Rais, Mtumba – Dodoma, kuhusu fursa za ushirikiano katika maendeleo ya biashara ya kaboni na utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia kwa ajili ya kulinda mazingira na kuchochea maendeleo endelevu.

Baadhi ya Watumishi wa Ofisi ya Makamu wa Rais wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu (Mazingira), Mhe. Balozi Baraka Luvanda (hayupo pichani) katika kikao kilichofanyika tarehe 15 Aprili 2026 katika Ofisi za Makamu wa Rais, Mtumba – Dodoma, kilicholenga kujadili fursa za ushirikiano katika maendeleo ya biashara ya kaboni na utekelezaji wa miradi ya nishati safi ya kupikia kwa ajili ya kulinda mazingira na kuchochea maendeleo endelevu.
=================================================================================================================
Naibu Katibu Mkuu (Mazingira) katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Balozi Baraka Luvanda, leo Aprili 15, 2026 amekutana na kufanya mazungumzo na wadau wa Mazingira katika Ofisi hizo zilizopo Mji wa Serikali Mtumba, jijini Dodoma.
Katika kikao hicho, pande zote mbili zimejadili fursa za kuanzisha na kuimarisha ushirikiano katika maeneo ya biashara ya kaboni, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Tanzania kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi pamoja na kunufaika na mifumo ya kimataifa ya kupunguza hewa ukaa.
Mazungumzo hayo yamegusia umuhimu wa kuendeleza matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa wananchi, ambapo pande zote mbili zimeonesha utayari wa kushirikiana katika kuhamasisha na kutekeleza miradi itakayochangia kupunguza utegemezi wa nishati zisizo rafiki kwa mazingira.
Balozi Luvanda amesisitiza kuhusu dhamira ya Serikali ya kuendelea kushirikiana na sekta binafsi katika kulinda mazingira, huku akieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kufikia malengo ya kitaifa na kimataifa ya uhifadhi wa mazingira na maendeleo endelevu.
Aidha, amewaomba wadau hao waendelee kushirikiana kwa karibu na Serikali ili kuhakikisha juhudi za Uhifadhi na utunzaji wa Mazingira zinatekelezwa kwa ufanisi na kuleta matokeo chanya kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Pia alisisitiza umuhimu wa elimu kwa umma kuhusu masuala ya Mazingira ili kuongeza uelewa na ushiriki wa wananchi katika kulinda rasilimali za asili.
Kwa upande wake William Davidson ambaye ni Mkurugenzi wa Freepoint, alisema kuwa nia ya kampuni yao ni kuendelea kuwekeza na kushirikiana na Tanzania katika miradi ya kimazingira, hususan inayohusiana na biashara ya kaboni na matumizi ya nishati safi ya kupikia.
Kikao hicho ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha ushirikiano na wadau mbalimbali katika kulinda mazingira na kuhakikisha matumizi endelevu ya rasilimali kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.