



==================================================================================
Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imepokea ujumbe kutoka Burkina Faso uliokuja nchini kwa lengo la kubadilishana uzoefu kuhusu masuala ya usimamizi wa mazingira katika shughuli za uchimbaji wa madini pamoja na taratibu za ufungaji wa migodi.
Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika Dodoma, Februari 19,2026 Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya udhibiti Uchafuzi Bw. Thomas Chali amesema lengo la kikao hicho ni kupata uelewa wa mfumo wa kisheria, kitaasisi na kiutendaji wa nchi ya Tanzania katika usimamizi wa kufunga migodi na urejeshaji wa maeneo yaliyoathiriwa na shughuli za uchimbaji madini.
Aidha pande zote mbili zilijadiliana kuhusu masuala mbalimbali ikiwemo tathmini za athari kwa mazingira, ufuatiliaji wa shughuli za kufunga migodi na udhibiti wa shughuli za uchimbaji wa madini.
Pamoja na hayo wawakilishi kutoka wizara ya madini walitoa maelezo kuhusu majukumu na wajibu wa wachimbaji wadogo na wakubwa katika utekelezaji wa shughuli za madini, kwa kuzingatia matakwa ya sheria na kanuni husika.
Ujumbe huo umeishukuru serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania hususani Ofisi ya Makamu wa Rais kwa mapokezi mazuri,ushirikiano na utayari wa kushirikisha uzoefu, maarifa na nyaraka muhimu kwa ajili ya kuimarisha usimamizi wa masuala ya madini na mazingira.